HABARI MPENZI MWANAMICHEZO KARIBU KATIKA KURASA HII MAHSUSI KWA HABARI ZA MICHEZO PIA UNAWEZA KUTANGAZA BIASHARA YAKO HAPA KWA BEI NAFUU ZAIDI KWA MUDA MREFU ZAIDI WASILIANA NASI KWA NAMBA +255713 15 33 48

3 April 2013

ZIARA YA KUTEMBELEA KLABU YA AJAX ILIVYOKUFA KIMAZIONGAOMBWE TFF !!!


HABARI mpenzi msomaji wa gazeti la hili pendwa bila shaka ni mzima wa afya. Leo nimeona niikumbushe ile ahadi aliyotoa Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo Dk. Emmanuel Nchimbi, wakati alipofanya ziara ya kutembelea ofisi za Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).

Waziri ambaye ni shabiki wa timu ya soka ya Majimaji ya Songea ‘Wanalizombe’ ya mkoani Ruvuma ambapo alifanya ziara katika vyama vya michezo ikiwemo ofisi za TFF.

 Kwa bahati nzuri, nilikuwa miongoni mwa waandishi waliokuwapo katika ziara hiyo, ambapo Waziri Nchimbi alianza kwa nasaha nyingi, lakini alipogusia kuhusu maendeleo ya soka, alikuwa amebeba mkoba wenye CD takriban tano hivi, alizopewa wakati alipokwenda ziarani jijini Amsterdam, Uholanzi ambako alipata bahati ya kutembelea yalipo makao makuu ya klabu ya Ajax, moja kati ya klabu kubwa duniani za soka kutoka barani la Ulaya.


Dk. Nchimbi hakuwa mchoyo alifungua CD mojawapo na kumpa Mkurugenzi wa Ufundi wa TFF, Sunday Kayuni, ambaye alitumia “projector” kuwaonyesha waandishi wa habari jinsi klabu hiyo inavyoweza kutengeneza wachezaji wake binafsi bila kushurutishwa na chama cha soka cha Uholanzi.

Nilivyotazama CD ile moyo wangu ukajibu ni ndoto kuifunga Ajax kwa mfumo wa kuzalisha vipaji tulionao kwani nyota wengi wa kipekee duniani wamepita pale kuanzia Johan Cruyff, Clarence Clyde Seedorf na wengine.

Nchimbi alitoa ofa kuwa TFF iteue jopo la watu watatu na wizara ili liende Uholanzi kutazama ambacho Ajax inakifanya ili baadaye watazame uwezekano wa kuingia mikataba na klabu hiyo kuja kuanzisha kituo cha michezo kwa ushirikiano na shirikisho la soka nchini humo.

Kwa bahati nzuri, waziri alikuwa na katibu wake siku hiyo pale pale alimpatia orodha ya watu wake ambao wangeenda Uholanzi lakini kwa TFF pengine ingekuwa mapema kwa dakika tano kufanya maamuzi, lakini cha kushangaza mpaka leo hii takriban miezi sita au nane sasa dalili za ziara hiyo sizioni wala kuchagua tu wa kwenda kujifunza utendaji wa Ajax katika maendeleo ya soka imekuwa kikwazo.

Swali ambalo linaniumiza kichwa ni hii TFF hata kuteua watu imekuwa shida, kuna tatizo gani? miongoni mwetu tunaifahamu timu ya Ajax Cape Town ya Afrika Kusini ambayo ninaamini ina mashirikiano makubwa na Ajax ya Uholanzi. Nafikiri hii ingekuwa bahati ya mtende kwetu kuchangamkia nafasi hii lakini maskini ya Mungu inaweza kuwa imeshamchafulia Waziri Nchimbi kuonekana mbabaishaji kule Uholanzi.

Waholanzi waliamua kumpa CD aone vipaji vinavyozalishwa lakini TFF haijajibu kile ilichotakiwa kufanya.

Kama wangekwenda Ajax na kutazama wanavyofanya wangeweza hata kuingia nao mikataba lakini; inaonyesha tutaishia kupeleka timu Ulaya kupata mazoezi kila siku. Haitasaidia hata kidogo nchi kama Tanzania niionavyo siyo ya kutaka kushiriki mataifa ya Afrika au Kombe la Dunia katika miaka kumi ijayo ni nchi ya kushiriki michuano 17 ijayo.


Eneo ninaloishi jirani zangu wakubwa ni Isack Mwakatika na Adolf Mohamed Rishard huwa wananiambia tatizo kubwa la Tanzania huwa tunajifananisha na Ulaya badala kujifananisha na Waafrika wenzetu; huwezi kushindanda na Ujerumani au Uingereza wakati nchi nyingi za Afrika zimetuzidi kiwango kwa kuwa zinafuata mfumo wa Ajax.

Nakubali mawazo yao hivi karibuni ya Kanali Kipingu alikuwa anaweza vipi kutengeneza wachezaji wa soka hata kama hawakuwa na matayarisho ya awali ya soka au baadhi ya watangazaji wa redio wakikusimulia walivyowaona wachezaji wakubwa duniani wanasema tofauti iliyopo kati yetu na wao ni kama mbingu na kaburi la futi 80.

Hata wachezaji wa Ligi Kuu ambao kutuliza mpira kwa mguu hawawezi, kwa jinsi hii TFF haina budi kwenda Ajax kuona mambo.

Au ushauri wa Nchimbi hamuutaki? TFF nawakumbusha nendeni Ajax hata kushangaa tu itawasaidia.

Ninaamini mkienda na kuzungumza nao tutayaona matunda ndani ya miaka mitano au kumi ijayo Safari njema mkienda.

No comments:

Post a Comment

lisungu_chisara@yahoo.com

TUTUMIE HABARI YOYOTE YA MICHEZO, BURUDANI TUTAZICHAPISHA

TANGAZA KWA MFUMO HUU


MAHUDHURIO YA WASOMAJI KIMATAIFA

free counters

Followers