HABARI MPENZI MWANAMICHEZO KARIBU KATIKA KURASA HII MAHSUSI KWA HABARI ZA MICHEZO PIA UNAWEZA KUTANGAZA BIASHARA YAKO HAPA KWA BEI NAFUU ZAIDI KWA MUDA MREFU ZAIDI WASILIANA NASI KWA NAMBA +255713 15 33 48

15 October 2013

Ujumbe wa Hija wa Walii Amri wa Waislamu wa Mwaka 1434 Hijria


Kwa jina la Allah Mwingi wa rehema Mwenye Kurehemu
Na hamdu na sifa zote njema ni za Mwenyezi Mungu Mola Mlezi wa viumbe vyote, na rehma na amani zimshukie Bwana wa Manabii na Mitume na Aali zake watukufu na masahaba zake wema.
Kuwadia kwa msimu wa Hija kunapasa kuhesabiwa kuwa ni Idi kubwa kwa umma wa Kiislamu. Ni fursa adhimu wanayopata Waislamu duniani katika masiku haya yenye thamani kubwa, na ni tiba ya kimiujiza ambayo kama itajulikana thamani yake na kama itatumiwa kama inavyostahiki, itakuwa dawa ya kuondoa madhara mengi yaliyousibu na yanayoweza kuusibu Ulimwengu wa Kiislamu.
Hija ni chemchemi ya rehma za Mwenyezi Mungu. Kila mmoja wenu nyinyi mahujaji mliopata saada, mnayo bahati hii kubwa ya kuzitumia amali hizi zilizojaa usafi na umaanawi kwa ajili ya kuzikosha nyoyo na roho zenu, na kuchukua kwenye hazina hii ya rehma, izza na nguvu akiba kwa ajili ya umri wenu wote uliobakia. Khushuu na unyenyekevu mnaouonyesha mbele ya Mwenyezi Mungu Mola Mrehemevu; ahadi mnayochukua ya kutekeleza majukumu waliyopewa Waislamu; uchangamko, harakati na uchukuaji hatua za kutekeleza mambo ya dini na dunia; kuwa na huruma na usamehevu katika kuamiliana na ndugu zenu; kuwa na ujasiri na moyo wa kujiamini katika kuyakabili matukio mazito; kuwa na matumaini ya kupata msaada na usaidizi wa Mwenyezi Mungu kila mahala na katika kila jambo; na kwa maneno mafupi ni kwamba mnaweza kuutumia uwanja huu wa mafunzo na malezi ya kidini wa kumwandaa Muislamu kwa ajili yenu wenyewe ili kuzipamba nafsi zenu kwa vito hivi na pia kuchukua kutoka kwenye hazina hizo zawadi kwa ajili ya nchi zenu, mataifa yenu na umma mzima wa Kiislamu.
Leo umma wa Kiislamu unahitajia kuliko kitu chochote kile kuwa na watu wanaoambatanisha fikra na matendo pamoja na imani, upendo na ikhlasi; na muqawama mbele ya maadui wenye kisasi sambamba na kuzijenga nafsi zao kimaanawi na kiroho. Hii ndio njia pekee ya kuiokoa jamii adhimu ya Waislamu na mazonge mbalimbali ya muda mrefu ambayo ama yanajulikana wazi kuwa yamesababishwa na adui au yametokana na udhaifu wa azma, imani na umaizi.
Hapana shaka kuwa zama hizi ni zama za mwamko na kurejea Waislamu kwenye utambulisho wao; uhakika huu unaweza kuonekana kwa uwazi kabisa kutokana na changamoto mbalimbali ambazo nchi za Waislamu zimekabiliana nazo. Na ni katika mazingira haya ambapo azma na irada inayotegemea imani, kutawakali, umaizi na tadbiri vinaweza kuyaletea ushindi na heshima mataifa ya Waislamu, na kuufanya mustakabali wao kuwa wenye izza na utukufu. Kambi wanayokabiliana nayo, ambayo haiwezi kuuvumilia mwamko na izza ya Waislamu imejitosa uwanjani kwa nguvu zake zote, na kutumia nyenzo zote za kiusalama, za kisaikolojia, za kijeshi, za kiuchumi na za kipropaganda kwa lengo la kuwavunja nguvu na kuwakandamiza Waislamu na kuwashughulisha wao kwa wao. Ukweli wa mengi unadhihirika kwa kutupia jicho hali ya nchi za Magharibi mwa Asia kuanzia Pakistan na Afghanistan hadi Syria, Iraq na Palestina, nchi za Ghuba ya Uajemi na vilevile nchi za kaskazini mwa Afrika kuanzia Libya, Misri na Tunisia hadi Sudan na nchi nyenginezo. Vita vya ndani, taasubi pogo za kidini na kimadhehebu; kukosekana uthabiti wa kisiasa; kuenea ugaidi wa kikatili; kujitokeza makundi na harakati zenye kufurutu mpaka za watu wanaovipasua vifua vya watu kwa namna zilivyokuwa zikifanya kaumu za kishenzi katika historia kisha kuutafuna kinyama moyo wa mtu; wanaobeba silaha na kuua watoto na wanawake; wanaowakata vichwa wanaume na kuwanajisi maharimu zao, na hata baadhi ya wakati wakatenda jinai hizi za kuaibisha na zenye kuchukiza kwa kutumia jina na bendera ya dini, yote hayo ni matokeo ya mpango wa kishetani na wa kiistikbari wa mashirika ya kiintelijinsia ya madola ya kigeni na maajenti wa tawala vibaraka yanazoshirikiana nazo katika eneo, na ambayo yanawezekana kujiri kutokana na mazingira yaliyoko ndani ya nchi mbalimbali na kuwaletea masaibu machungu wananchi wa mataifa hayo. Ni hakika kwamba katika hali na mazingira kama haya haiwezekani kutarajia kuwa nchi za Waislamu zitaweza kufanya marekebisho kwa kujaza fursa tupu za kimaada na kimaanawi na kupata amani, ustawi na maendeleo ya kielimu na uwezo imara kimataifa ambavyo ni matunda ya baraka za mwamko na kurejea kwenye utambulisho wao. Hali hizi za kuhuzunisha zinaweza kuviza Mwamko wa Kiislamu na kuupoteza utayarifu wa kiroho uliopatikana katika Ulimwengu wa Kiislamu; na kwa mara nyengine tena kuyaweka mataifa ya Waislamu katika hali ya kuzorota, kutengwa na kuporomoka kwa miaka mingine mingi, na kuyasahau masuala yao ya msingi na muhimu kama kuiokoa Palestina na kuyaokoa mataifa ya Waislamu na unyang'anyi wa Marekani na Uzayuni.
Dawa mujarabu na ya msingi inaweza kupatikana katika ibara mbili muhimu ambazo zote ni miongoni mwa mafunzo ya wazi kabisa ya Hija:
Mosi: Umoja na udugu wa Waislamu chini ya bendera ya tauhidi.
Pili: Kumtambua adui na kukabiliana na njama na mbinu zake.
Kuimarisha moyo wa udugu na mshikamano ni funzo kubwa la Hija. Katika mahala hapo ni marufuku hata kubishana na kuwatolea maneno watu wengine. Kuvaa vazi la aina moja, kufanya amali za namna moja na harakati za aina moja, na kuwa na tabia ya huruma katika mahala hapo kunamaanisha usawa na udugu wa watu wote wenye imani na wenye kufungamana na mhimili wa tauhidi. Hili ni jibu la wazi kabisa la Uislamu kwa kila fikra, itikadi na wito unaolitoa nje ya Uislamu kundi mojawapo la Waislamu wenye imani na Ala Kaaba na tauhidi. Watu wakufurishaji, ambao leo hii wamekuwa vikaragosi wa kutekeleza siasa za Wazayuni mahaini na waungaji mkono wao wa Magharibi, na ambao wanatenda jinai kubwa na kumwaga damu za Waislamu wasio na hatia; pamoja na wale wanaojidai kuwa Waswalihina na wale wanaojivika vazi la ushekhe, ambao wanakoleza moto wa hitilafu baina ya Shia na Suni na mfano wa hayo, wajue kwamba amali yenyewe ya Hija inayabatilisha madai yao. La kustaajabisha; wale watu ambao mkusanyiko wa kujibari na washirikina ambao asili yake inatokana na amali ya Mtume Mtukufu SAW wanauchukulia kuwa ni katika mabishano yaliyokatazwa, wao wenyewe wako mstari wa mbele katika kuchochea mizozano ya umwagaji damu kati ya Waislamu.
Mimi, kama walivyo maulama wengine wa Uislamu na wenye uchungu na umma wa Kiislamu, kwa mara nyengine tena ninatangaza kuwa, kauli yoyote na kitendo chochote kitakachosababisha kuwashwa moto wa hitilafu baina ya Waislamu, na vilevile kuyatusi matukufu ya lolote lile kati ya makundi ya Waislamu, au kuikufurisha mojawapo kati ya madhehebu za Kiislamu, ni kuitumikia kambi ya ukafiri na shirki na ni usaliti kwa Uislamu na ni haramu kidini.
Kumtambua adui pamoja na mbinu zake ndio nguzo ya pili. Kwanza kabisa haifai kughafilika na kusahau kwamba kuna adui mwenye kisasi; na amali ya mara kadhaa ya kumrembea mawe Shetani huko Jamarati katika Hija ni alama ya mfano wa kulikumbuka jambo hilo akilini muda wote. Pili, haitakiwi kufanya makosa katika kumtambua adui wa asili, ambaye leo hii ni hiyo kambi ya Uistikbari wa dunia na mtandao mtenda jinai wa Uzayuni; na tatu, inapasa kuzielewa vizuri mbinu zinazotumiwa na adui huyu mwenye inadi, ambazo ni kuchochea mifarakano baina ya Waislamu, kueneza ufisadi wa kisiasa na kiakhlaqi, kuwatisha na kuwarubuni wenye vipawa, kutoa mashinikizo ya kiuchumi kwa mataifa, na kueneza shaka katika imani za Kiislamu; na vilevile kuwatambua vibaraka na wasaidizi wao, ambao kwa kujua au kwa kutojua, wanawasaidia katika njia.
Madola ya Kiistikbari, na la mbele kabisa Marekani, yanatumia msaada wa nyenzo za vyombo vingi na vya kisasa vya habari ili kuficha sura yao halisi; na huku yakijidai kuwa waungaji mkono wa haki za binadamu na demokrasia huonyesha muamala wa kutaka kuzihadaa fikra za waliowengi katika mataifa. Huwa yanadai kutetea haki za mataifa katika hali ambayo, zaidi ya ilivyokuwa huko nyuma, mataifa ya Waislamu yanauhimili kila siku kwa mwili na roho zao moto wa fitina unaowashwa na madola hayo. Kwa kulitupia jicho taifa madhulumu la Palestina ambalo kwa miaka na miaka linaenedelea kupata majeraha ya jinai za utawala wa Kizayuni na waungaji mkono wake; au nchi za Afghanistan, Pakistan na Iraq ambazo maisha ya wananchi wao yamekuwa machungu kutokana na ugaidi ulioletwa na siasa za Uistikbari na wasaidizi wake wa eneo, au nchi ya Syria, ambayo kwa kosa la kuunga mkono harakati ya muqawama dhidi ya Uzayuni inaandamwa na wimbi la uadui la mabeberu wa kimataifa na watendaji wao wa eneo na kutumbukizwa kwenye vita vya ndani vya umwagaji damu, au nchi za Bahrain au Myanmar, ambazo kila moja kwa namna yake, Waislamu wanaoteseka wamesahauliwa, na maadui zao wanasaidiwa na kuungwa mkono, au kwa kuyaangalia mataifa mengine ambayo yanaandamwa na mashambulio mtawalia ya kijeshi, au vikwazo vya kiuchumi au hujuma za kiusalama, yote hayo yanaweza kuwadhihirishia watu wote sura halisi ya viranja hao wa mfumo wa ubeberu.
Wenye vipawa vya kisiasa, vya kiutamaduni na vya kidini wa kila mahala katika Ulimwengu wa Kiislamu wajijue kwamba wana wajibu wa kuufichua ukweli huu. Hili ni jukumu letu sote la kiakhlaqi na kidini. Nchi za kaskazini mwa Afrika, ambazo kwa masikitiko leo hii zimekumbwa na hitilafu kubwa za ndani zinapaswa kulizingatia zaidi jukumu hili adhimu, yaani kumtambua adui, mbinu na hila zake. Kuendelea hitilafu baina ya mirengo ya kitaifa na kughafilika na hatari ya vita vya ndani katika nchi hizi ni hatari kubwa ambayo hasara yake kwa umma wa Kiislamu haitoweza kufidika haraka.
Sisi, bila ya shaka hatuna shaka kwamba wananchi wa mataifa ya eneo waliosimama kidete wakautekeleza kivitendo Mwamko wa Kiislamu, kwa idhini ya Mwenyezi Mungu hawatoruhusu alama za nyakati zirudi nyuma na kurejea tena zama za watawala waovu, vibaraka na madikteta; lakini kughafilika na nafasi ya madola ya Kiistikbari katika kuzusha fitina na uingiliaji wao wa uharibifu kutaifanya kazi yao iwe ngumu na kuzirudisha nyuma kwa miaka na miaka zama za izza, amani na ustawi. Sisi tuna imani ya dhati ndani ya nyoyo zetu juu ya uwezo wa mataifa na nguvu ambazo Mwenyezi Mungu Mwenye hekima ameupa umma wa wananchi katika azma, imani na umaizi; na hilo tumejionea kwa macho yetu na kupata tajiriba kwa nafsi zetu kwa zaidi ya miongo mitatu katika Jamhuri ya Kiislamu ya Iran; tunachojitahidi kufanya ni kutoa wito kwa mataifa yote ya Waislamu wa kuifuata tajiriba hii ya ndugu zao katika nchi hii yenye heshima na isiyochoka.
Ninamwomba Mwenyezi Mungu Mtukufu yale yenye maslaha kwa Waislamu na kuwakinga na vitimbi vya maadui. Na ninamwomba akutakabalieni Hija yenu nyinyi nyote mahujaji wa Nyumba ya Mwenyezi Mungu, na akupeni uzima wa kimwili na kiroho na atiya ya akiba kubwa ya kimaanawi.
Wassalamu Alaykum Warahmatullahi Wabarakatuh
Sayyid Ali Khamenei
Tarehe 5 Dhilhijjah 1434 inayosadifiana na tarehe 19 Mehr 1392

No comments:

Post a Comment

lisungu_chisara@yahoo.com

TUTUMIE HABARI YOYOTE YA MICHEZO, BURUDANI TUTAZICHAPISHA

TANGAZA KWA MFUMO HUU


MAHUDHURIO YA WASOMAJI KIMATAIFA

free counters

Followers