HABARI MPENZI MWANAMICHEZO KARIBU KATIKA KURASA HII MAHSUSI KWA HABARI ZA MICHEZO PIA UNAWEZA KUTANGAZA BIASHARA YAKO HAPA KWA BEI NAFUU ZAIDI KWA MUDA MREFU ZAIDI WASILIANA NASI KWA NAMBA +255713 15 33 48

5 April 2014

ODEN MBAGA AREJESHWA DARASA UPYA


 

Kamati ya Maadili ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) imesikiliza malalamiko dhidi ya waamuzi wa FIFA, Oden Mbaga na Samwel Mpenzu na kuagiza wakafanye upya mitihani ya utimamu wa mwili (physical fitness test) katika robo (quarter) inayofuata.

Katibu Mkuu wa TFF alikuwa amewalalamikia waamuzi hao pamoja na Mkufunzi wa CAF, Riziki Majala na Mkufunzi wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mchungaji Army Sentimea kwa kuwafanyisha waamuzi hao mtihani huo kinyume na utaratibu ikiwemo pia kughushi matokeo.

Waamuzi hao wametakiwa kufanya mtihani huo katika robo inayofuata ambapo wakifaulu waendelee kuchezesha mechi. Waamuzi wa FIFA hufanya mitihani hiyo mara nne kwa mwaka.

Mbaga alifeli mtihani wa robo ya nne uliofanyika Desemba mwaka jana wakati Mpenzu hakufanya kabisa kwa vile alikuwa mgonjwa. Baadaye Majala aliwafanyisha mtihani mwingine waamuzi hao ambao haukutambuliwa na TFF kwa vile uliandaliwa kinyume cha taratibu, huku Mkufunzi huyo akidai ana mamlaka ya kuandaa mafunzo hayo.

Kamati hiyo iliyokutana jana (Aprili 4 mwaka huu) chini ya Mwenyekiti wake William Erio, imesema imebaini hakuna utaratibu unaoeleweka wa kuendelesha mitihani hiyo, hivyo kuagiza TFF kufanyia kazi suala hilo ili kubainisha mamlaka na mipaka ya kila mhusika wakiwemo wakufunzi.

Vilevile Kamati ilibaini kuwa Mchungaji Sentimea hakuhusika kwa lolote katika uendeshaji wa mtihani huo ulioandaliwa na Majala, hivyo kumuondoa kwenye malalamiko hayo.

Kwa upande wa Ofisa Takwimu wa TFF, Sabri Mtulla ambaye alilalamikiwa kwa kuidanganya Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji kuwa hakukuwa na pingamizi dhidi ya mchezaji Emmanuel Okwi wakati wa kipindi cha usajili wakati akijua lilikuwepo, Kamati ya Maadili imeagiza suala hilo liwasilishwe kwao upya pamoja na ushahidi wa kuthibitisha kama kweli mlalamikiwa alifahamu juu ya suala hilo.

Mtulla alijitetea mbele ya Kamati ya Maadili kuwa hakuwahi kuona wala kukabidhiwa barua ya Simba iliyokuwa ikipinga usajili wa Okwi katika klabu ya Yanga.

YANGA YAMLALAMIKIA STRAIKA WA MGAMBO SHOOTING
Klabu ya Yanga imewasilisha malalamiko Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) kuwa mshambuliaji wa Mgambo Shooting Stars ambaye alicheza dhidi yao katika mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom (VPL), Mohamed Neto si raia wa Tanzania na hana Hati ya Uhamisho wa Kimataifa (ITC).

Ingawa malalamiko hayo yamewasilishwa nje ya muda (time barred), TFF imeyapokea na itayawasilisha kwenye Kamati husika kwa ajili ya kupitiwa na baadaye kutolewa uamuzi.

Kwa mujibu wa kanuni, malalamiko yote kuhusu mchezo yanatakiwa kuwasilishwa ndani ya saa 24 baada ya mchezo kumalizika.

No comments:

Post a Comment

lisungu_chisara@yahoo.com

TUTUMIE HABARI YOYOTE YA MICHEZO, BURUDANI TUTAZICHAPISHA

TANGAZA KWA MFUMO HUU


MAHUDHURIO YA WASOMAJI KIMATAIFA

free counters

Followers