HABARI MPENZI MWANAMICHEZO KARIBU KATIKA KURASA HII MAHSUSI KWA HABARI ZA MICHEZO PIA UNAWEZA KUTANGAZA BIASHARA YAKO HAPA KWA BEI NAFUU ZAIDI KWA MUDA MREFU ZAIDI WASILIANA NASI KWA NAMBA +255713 15 33 48

19 November 2012

Swahili Hiphop ndani ya Alliance Française tarehe 22


Kampuni ya ASAR Entertaiment ikishirikiana na Ubalozi wa Switzerland na Kituo cha Ufaransa cha Utamaduni, Alliance Française de Dar es Salaam, inakuletea maonyesho ya Swahili Hiphop 2012 yatakayofanyika kwa siku nzima kwenye viwanja vya Alliance Française siku ya alhamisi ya tarehe 22 ya mwezi huu.



Maonyesho haya ni bure, kwa maana kwamba hakuna kiingilio, na bidhaa zitakazoonyeshwa ni zile zinazotengenezwa na wasanii wa hiphop au vikundi mbalimbali vya vijana wa Kitanzania, kama vile CDs (santuri), kanda mseto, majarida, posters, mavazi, bidhaa mbalimbali za kitamaduni na kadhalika, lengo likiwa kuwapa nafasi ya bure ya kuonyesha na kuuza kazi zao.



Pamoja na mauzo hayo yatakayofanywa na wasanii arobaini wa hiphop, pia kutakuwa na mafunzo ya nguzo tano za hiphop yatakayotolewa na wakufunzi waliobobea katika nyanja hizo, ikiwemo vipindi vya u-dj, utunzi wa mashairi, utengenezaji wa ala za muziki, upigaji machata (graffiti) na mabreka (breakdancing), ikifuatiwa na burudani mbalimbali za u-MC zitakazotolewa na wasanii wakongwe na mahiri wa hiphop.



Maonyesho haya yataanza rasmi Saa Tatu asubuhi mpaka Saa Nne usiku, ikifuatiwa na siku nzima (Ijumaa, 23 / 11 / 2012) ya Swahili Hiphop Summit 2012, mkutano utakaofanyika katika ukumbi wa Alliance Française, tarehe 23 kuanzia saa mbili asubuhi mpaka saa tisa alasiri.



Mkutano huu utafunguliwa na balozi wa Switzerland nchini Tanzania, Mr. Olivier Chave na utahudhuriwa na  wageni waalikwa wapatao 200, wakiwemo mabalozi wa nchi mbalimbali, viongozi wa serikali, wakurugenzi wa mashirika, wafanyabiashara, wadau mbalimbali wa muziki, wazazi, mashabiki na wasanii wa muziki kwa ujumla, hususan wale wa hiphop.



Lengo kuu la mkutano huu ni kujadili changamoto mbalimbali zinazoikumba tansia ya muziki wa hiphop na njia za kutatua matatizo haya ambayo pia yanawakumba wasanii wengine wasiofanya muziki wa hiphop.



Mijadala mbalimbali itaendeshwa katika kufikia malengo ya kuwakomboa wanamuziki hawa, ikiwemo suala zima la haki za wasanii, hati miliki, muziki kama biashara na maisha, na hata tafsiri mbovu juu ya neno ‘hiphop’. Mkutano huu utakamilishwa na kilingi cha wanamuziki wa hiphop, ama cypher kwa lugha ya kimombo, itakayofanyika kwa kutumia midundo ya ngoma za kitamaduni.



Pia jioni ya ijumaa hiyo, tarehe 23 / 11 kwanzia saa kumi na moja jioni, kutakuwa na shoo kali ya uzinduzi wa santuri ya msanii mpya wa hiphop aendae kwa jina la Randy ‘D Dawn kutoka kundi la Watanzah, atakayepanda jukwaani kwa kishindo akisindikizwa na kundi lake hilo.

Shoo hii ni bure kwa wote.  Steji pia itashambuliwa na wasanii wengine hatari katika hiphop akiwemo JCB na Mo Plus kutoka jijini Arusha, Juma Nature, Imam Abbas, Salu T na msanii matata kutoka nchni Ghana aitwaye Lucci Mo.



Tamasha hili, maonyesho ya Swahili Hiphop 2012 pamoja na Swahili Hiphop Summit 2012 yanaletwa kwenu kwa udhamini wa Ubalozi wa Switzerland nchini Tanzania, Alliance Française de Dar es Salaam, NSSF, Clouds FM, JD’s Entertainment, gazeti la MwanaSpoti, na Swahili Hiphop Family Club.



MAHALI: ALLIANCE FRANCAISE DE DAR ES SALAAM

TAREHE: 22 & 23 NOVEMBA 2012 / Kwanzia saa 3asubuh / BURE

Mawasiliano: swahilihiphopsummit@gmail.com / +255 713 300 080

No comments:

Post a Comment

lisungu_chisara@yahoo.com

TUTUMIE HABARI YOYOTE YA MICHEZO, BURUDANI TUTAZICHAPISHA

TANGAZA KWA MFUMO HUU


MAHUDHURIO YA WASOMAJI KIMATAIFA

free counters

Followers